Serikali Yatoa Milion 402 Kwa Ajili Ya Utekelezaji Wa Mradi Wa Maji Singiwe.



Na Baraka Lusajo - Kalambo.

Serikali katika lengo lake la kumtua mama ndoo kichwani, imetoa fedha kiasi cha shilingi milioni 402 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji ambayo inatarajiwa kuhudumia vijiji 11 vyenye zaidi ya wananchi elfu sita (6000) katika Halmashauri ya wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa na kuwaondolea adha wananchi kutembea umbali mrefu kufuata huduma hiyo katika mto Mzwalo.

Meneja wa RUWASA wilayani Kalambo Patrick Ndimbo, amesema mradi wa Singiwe ulianza kutekelezwa Julay 25/2020 na makadirio ya mradi ilikuwa ni shilingi 416,891,454 na kutakiwa kutekelezwa kwa muda wa miezi mitatu.

‘’Kabla ya ujenzi wa mradi huu hapakuwa na huduma ya uhakika ya maji, kwa kuwa mradi uliokuwepo ulikuwa wa miaka mingi na miundomdombinu yake ilikuwa chakavu sana. Pia kazi zilizofanyika katika mradi huu mpya ni sawa na asilimia 50% na mpaka sasa tumetumia fedha kiasi cha shilingi million 170,524,282 sawa na asilimia 41% ya makadirio ya mradi wote.

Mkuu wa TAKUKURU wilayani humo Lupakisyo Mwakyolile, amesema mradi huo wanaufuatilia kwa ukaribu lengo likiwa ni kuhakikisha unakamilika kwa  wakati na kuwawezesha wananchi kunufaika na huduma hiyo muhimu.

Akiongea mara baada ya kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo kutembelea na kukagua mradi huo, mkuu wa wilaya hiyo Calorus Misungwi, amesema ujenzi wa miradi hiyo itawawezesha kupata maji safi na salama kwa wakati wote na kuwasihi watumiaji wa maji kulinda miradi hiyo ili iweze kudumu kwa muda mrefu.

Ili kuwa na miradi endelevu ya RUWASA wilaya ya Kalambo  kwa kushirikiana  na ofisi ya Mkurugenzi mtendaji kupitia idara ya maji (CBWSO) inayojulikana kwa jina la Jumuhiya ya watumiaji maji Mzwalo ambayo itasimamia uendeshaji wa matengenezo ya mradi wa maji Singiwe pindi ukikamilika.

 

 

Comments