Na Baraka Lusajo - Rukwa
Mkoa wa Rukwa umezindua zoezi la utoaji chanjo ya polio kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano ambapo imelenga kuwafikia watoto 217,674 katika wilaya za Sumbawanga, Nkasi na Kalambo.
Mkuu wa Mkoa huo Joseph
Mkirikiti leo (18.05.2022) amezindua kampeni hiyo katika kituo cha afya Mazwi
kilichopo Manispaa ya Sumbawanga na kutoa rai kwa wazazi kuwapeleka watoto
kupata chanjo hiyo ambayo itawakinga dhidi ya ugonjwa wa kupoza.
“Wazazi jitokezeni kupeleka
watoto kwenye vituo vya afya ili wapate chanjo hii ya polio ambayo ni salama na
itawakinga dhidi ya ugonjwa wa kupoza. Madhara ya polio ni hatari, hivyo
tuwalinde watoto wetu ili waendelee kuwa salama” alisema Mkirikiti.
Mkirikiti alieleza kuwa wazazi wawe mabalozi kwa wenzao wenye watoto chini ya miaka mitano kuhamasisha washiriki zoezi hilo ambalo linafanyika kote katika vituo vya afya mkoani Rukwa.
Akitoa taarifa ya kampeni
hiyo kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Mkoa, Mratibu wa Huduma za Afya ya Uzazi, Mama
na Mtoto mkoa wa Rukwa Asha Izina alisema mkoa umepanga kuchanja watoto walio
na umri chini ya miaka mitano wapatao 217,674 kutoka katika halmashauri nne za
Rukwa.
Mratibu huyo aliongeza
kusema maandalizi yamekamilika ambapo tayari watoa huduma 504 watakaoshiriki
zoezi la uchanjaji wametakiwa mafunzo na kuwa mkoa umepokea chanjo dozi 250,320
na vifaa vingine.
Naye Mganga Mkuu wa Manispaa
ya Sumbawanga Dkt. Sebastian Siwale alisema polio ni ugonjwa unaosababisha
watoto kupoza hivyo akitoa wito kwa wazazi na walezi kuwapeleka watoto kwenye
vituo vya afya kupata chanjo hii muhimu.
Dkt. Siwale aliwatoa hofu wazazi kuwa chanjo hii haina madhara kwani imekuwa ikitolewa siku zote kwenye kliniki kwa watoto lakini kutokana na nchi jirani ya Malawi kuwa na mlipuko wa ugonjwa huu, Serikali imelazimika kuendesha kampeni hii ili kuwafikia watoto wengi zaidi.
Akizungumza na waandishi wa
habari mmoja wa wazazi aliyejitokeza kwenye zoezi hilo Bahati Juma mkazi wa
Sumbawanga alisema baada ya kusikia matangazo kwenye redio ndipo akaamua
kumpeleka mtoto wake ili apate chanjo ya polio ili asije ambukizwa ugonjwa huo.
Kampeni ya polio imeanza leo
na itachukua muda wa siku nne hadi tarehe 21 Mei mwaka huu itakapohitimishwa
katika halmashauri za Sumbawanga Manispaa, Sumbawanga vijijini, Kalambo na
Nkasi,
Comments
Post a Comment