Na
Baraka Lusajo – Rukwa.
Mkoa wa Rukwa umefanikiwa kusajili na kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto 124,498 chini ya mpango wa Usajili wa watoto walio na umri chini ya miaka mitano unaoratibiwa na Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA) ulioanza Novemba mwaka 2021.
Mafanikio
hayo yamebainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti jana (16 Mei, 2022) wakati akifungua kikao
cha tathmini kuhusu utekelezaji wa mpango huo kilichofanyika mjini Sumbawanga.
“Mkoa
wetu katika mpango huu tumesajili watoto 124,498 sawa na asilimia 47.7 ya lengo
la kusajili watoto 263,239. Ikumbukwe kwamba kabla ya kuanza mpango huu hapo
Novemba 2021 tulikuwa na asilimia 5.8 hivyo tumeongeza usajili wa watoto kwa
asilimia 41.9 “alisema Mkirikiti.
Mkirikiti alibainisha changamoto kuwa cheti cha kuzaliwa kinatolewa kwa watu waliozaliwa katika ardhi ya Tanzania pekee na kutokana na mkoa wa Rukwa kuwa na mwingiliano mkubwa wa wananchi wa nchi jirani imekuwa ngumu kuwatambua wanaostahili kusajiliwa na kupata nyaraka.
Katika
hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa alitoa wito wananchi kuendelea kujitokeza
kusajili watoto wao chini miaka mitano kwa kuwa cheti kinatolewa bure na hakuna
fedha yoyote mwananchi atakayochangia.
Kwa
upande wake Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini
(RITA) Charles Salyeem alisema Mpango huo umeleta maboresho makubwa katika
mfumo wa usajili wa vizazi na kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto kwani sasa
huduma hiyo inapatikana katika Ofisi za Watendaji Kata na Vituo vya Tiba kote
mkoani Rukwa.
Salyeem alisema pia RITA kupitia mpango huo (Under 5 Birth Registration Iniative-U5BRI) ulioanza Novemba22, 2021 umefanikiwa kusajili na kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto Milioni 7.5 katika mikoa 22 ya Tanzania Bara ambapo kiwango cha usajili kimeongezeka toka asilimia 13 hadi kufikia asilimia 65.
Alitaja
changamoto ya wazazi wengi kutokuwa na Kitambulisho cha Taifa kuwa ni kikwazo
cha watoto wengi kufikiwa, hata hivyo RITA kwa kushirikiana na Wakala wa
Vitambulisho vya Taifa (NIDA) wanaendelea kutafuta ufumbuzi wa changamoto hiyo.
Mpango
huu unatekelezwa na RITA kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la
Kuhudumia Watoto Duniani (UNICEF), Serikali ya Canada, NIDA, Uhamiaji, OR-
Tamisemi na kampuni ya Simu za Mikononi ya TIGO.
Kikao
hicho cha tathmini kimehudhuriwa na wakuu wa wilaya za Sumbawanga, Nkasi na
Kalambo, wajumbe wa kamati ya usalama mkoa, wakurugenzi wa halmashauri,
Makatibu Tawala wilaya, viongozi wa dini na mila , Maafisa Ustawi wa Jamii
pamoja na Waganga wakuu wa Wilaya zote za mkoa wa Rukwa.
Mpango
huu kwa mikoa ya Rukwa na Katavi ulizinduliwa kwa mara ya kwanza Novemba 25
mwaka 2021 na aliyekuwa Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi
mkoani Katavi.
Comments
Post a Comment