Baraka lusajo – Rukwa.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph
Mkirikiti amezionya halmashauri za mkoa huo kwa kutokutoa fedha za utekelezaji
wa afua za lishe katika kipindi cha Octoba hadi Desemba 2021.
Ametoa onyo hilo jana (25.02.2022) wakati akiongoza kikao cha tathmini ya mkataba wa shughuli za lishe kipindi cha Julai hadi Desemba 2012 kilichofanyika mjini Sumbawanga ambapo halmashauri zote nne ziliripotiwa kutoa fedha za lishe asilimia 17.5 tu hatua inayokwamisha shughuli za lishe.
“Leo ndio siku ya mwisho
nisisikie kuwa Afisa Lishe anasema hajapewa fedha za kutekeleza shughuli wakati
mkoa bado una tatizo la udumavu na utapiamlo .Wakurugenzi nendeni mkabadilike
.Suala la lishe ni agenda muhimu kwa uhai wa watu wetu pamoja na watoto wetu” alisisitiza Mkirikiti.
Kwa mujibu wa taarifa
iliyotolewa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa ambaye pia ni Mganga Mkuu wa Mkoa wa
Rukwa Dkt. Bonoface Kasululu ilionyesha kuwa halmashauri za Sumbawanga
Manispaa, Sumbawanga Vijijini, Nkasi na Kalambo zimetoa asilimia 17 na
kupelekea mkoa uwe kwenye rangi nyekundu.
Dkt. Kasululu aliongeza
kusema matokeo ya ujumla yanaonesha kuwa mkoa wa Rukwa una wastani wa alama
asilimia 87 ambapo kiasi hicho kimechangiwa na kutokutolewa kwa fedha za afua
za lishe kwa upande wa halmashauri.
“Asilimia ya bajeti ya
halmashauri iliyotumika kutekeleza shughuli za lishe kati ya iliyotengwa rangi
nyekundu ni asilimia 17.5 kiashiria hiki kinaendelea kufanya vibaya zaidi
ikilinganishwa na matokeo ya asilimia 54 kipidi cha mwaka 2020/2021” alieleza
Dkt. Kasululu.
Taarifa ya tathmini kwa
kiashiria cha asilimia ya fedha zilizotumika kwa shughuli za lishe katika
kipindi cha Julai hadi Desemba 2021 kwenye halmashauri na asilimia zake kwenye
mabano Manispaa ya Sumbawanga (0.0), Sumbawanga DC (18.9), Nkasi DC (0.0) na
Kalambo DC (47.7) hatua inayofanya mkoa kuwa na jumla ya asilimia 17.5
Mmoja wa Maafisa Lishe toka
Halmashauri ambaye hakutaka jina litajwe alisema “tumekuwa tukiandika madokezo
kuomba fedha za shughuli za lishe lakini hatupatiwi bila kupewa sababu. Octoba
–Desemba 2021 niliomba shilingi 800,000
lakini hadi leo sijajibiwa na kazi zimesimama” alisema mtaalam huyo.
Kwa upande wake Mwakilishi
wa Shirika la Jukwaa la Lishe Tanzania (PANITA) Aron Isaack alisema licha ya
mkoa wa Rukwa kushika nafasi ya 13 kati 26 mwaka 2020/21 bado kuna changamoto
kubwa ya shughuli za lishe kutopewa kipaumbele hatua inayosababisha utapiamlo
na udumavu kuendelea.
Isaack aliongeza kuwa
kunahitajika utashi wa kisiasa ili kutekelezwa kwa mkataba wa lishe miongoni
mwa viongozi na watendaji wa serikali wakiwemo Waganga Wakuu wa Wilaya za
Rukwa.
“Tunaishukuru serikali kwa
kusimamia suala la lishe hasa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020
iliyotamka suala la lishe kupewa kipaumbele “alisema Isaack.
Alisema lengo la serikali ni
kuhakikisha watoto hususani wenye umri chini ya miaka 5 wakuwa na lishe bora na kufikia maelengo y kutokomeza uduma kwa watoto ambao ni taifa la kesho.
Kwa mujibu wa taarifa ya
lishe iliyotolewa na Wizara ya Kilimo Desemba 2020 ilionesha kuwa mikoa
inayoongoza kwa uzalishaji mazao ya chakula ndio ina kiwango kikubwa cha
udumavu unaotokana na utapiamlo ikiwemo Rukwa (47.9), Njombe (53.6) na Iringa
(47.1) huku watoto wenye umri chini ya miaka 8 wakitajwa kuathirika zaidi na tatizo la udumavu.
Mwisho.
Comments
Post a Comment