SERIKALI YA IDHINISHA BILION 1.3 KWA AJILI YA UJENZI WA MIRADI 4 YA MAJI MKOANI RUKWA.


Na Baraka Lusajo - Rukwa.

Wakandarasi wanaotekeleza miradi ya maji mkoani Rukwa wametakiwa kuwa waadilifu na wazalendo ili wananchi wapate maji vijijini na mijini kwa ustawi wa jamii hatua itakayo ondoa kero za ukosefu wa maji.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti wakati aliposhuhudia hafla ya utiaji saini mikataba minne ya miradi ya maji kwa kati ya Wakala  wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) na wakandarasi mjini Sumbawanga.

“Miradi hii haihitaji stori, tunahitaji siku 180 za mkataba zitumike kukamilisha ujenzi wa miradi ya maji huku tukizingatia matumizi sahihi ya fedha pamoja na uadilifu “alisema Mkirikiti.

Katika hafla hiyo mikataba minne ya ujenzi wa miradi ya maji yenye thamani ya shilingi 1,383,238,518 itakayotekelezwa kwa siku 180 katika wilaya za Nkasi na Sumbawanga.

 

Akitoa taarifa kabla ya utiaji saini, Meneja wa Mkoa wa Wakala wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Mhandisi Boaz Matundali alisema jumla ya miradi 19 imetangazwa katika mwaka huu wa fedha ambapo minne kati yake imepata wakandarasi.

 

Mhandisi Boaz alitaja miradi itakayosainiwa kuwa ni ujenzi wa mradi wa maji Msanda Muungano wilaya ya Sumbawanga wenye thamani ya shilingi Milioni 295.7 chini ya mkandarasi Kiluswa Building Contrators ya Sumbawanga.

 

Miradi mengine itatekelezwa katika wilaya ya Nkasi ambayo ni ujenzi wa mradi wa maji Lyazumbi  (shilingi Milioni 308.4), ujenzi wa mradi wa maji Kacheche (shilingi Milioni 385.0) na mradi wa maji Masolo (shilingi Milioni 395.9) yote itatekelezwa na mkandarasi Consel Construction and Engineering Services ya Mwanza.

 

Katika hatua nyingine Mhandisi Boaz alisema katika mwaka huu RUWASA mkoa wa Rukwa unatumia wakandarasi katika kutekeleza miradi yake tofauti na ilivyokuwa mwaka uliopita ambapo miradi ilitumia force account na nguvu za wananchi hivyo wanategemea itakamilika ndani ya kipindi cha siku 180 za mkataba.

Comments