Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti ameagiza Wakuu wa Wilaya za mkoa huo kuhakikisha wanafuatilia na kudhibiti kuongezeka kwa wanafunzi wa kike wanaokatisha masomo kutokana na tatizo la mimba.
Akizungumza
mjini Sumbawanga Mkuu huyo wa Mkoa alionesha kutofurahishwa na kasi ya
kuongezeka kwa wanafunzi wa kike wanaoshindwa kukamilisha masomo yao sababu
ikitajwa kuwa ni kupata ujauzito.
“Lazima tuongeze mapambano kudhibiti mimba za utotoni .Sijafurahishwa kuona wilaya ya Nkasi ikiwa na idadi ya wanafunzi Ishirini Tano (25) mwaka huu waliopata mimba wakiwa wanasoma. Hii haikubaliki. Wakuu wa wilaya nendeni mkadhibiti vitendo hivi” alisisitiza Mkirikiti.
Takwimu
za Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa zimeonesha kuwa katika mwaka huu 2021 wilaya ya
Nkasi imekuwa na matukio 25 ya wanafunzi wa kike kupata mimba huku wilaya ya
Kalambo ikiripoti wasichana wanane (8) na Wilaya ya Sumbawanga nayo ikiwa na wanafunzi
wanane (8).
Mkirikiti
aliagiza pia Maafisa Elimu Kata kutimiza majukumu yao kwa kufuatilia walimu na
watu wanaojihusisha na kuwapatia mimba wanafunzi kwani zipo taarifa baadhi ya
walimu wanahusika na vitendo hivyo kinyume na maadili ya kazi.
“Maafisa Elimu Kata mmepewa pikipiki na serikali ili zitumike kutekeleza majukumu ya kusimamia elimu kwenye mashule ikiwemo kufuatilia wazazi na walezi wasiolea watoto wao hatua inayopelekea baadhi ya watoto wa kike kupata mimba na watoto wengine kuacha shule bila sababu” alisitiza Mkirikiti.
Aidha, Mkirikiti amemwagiza Afisa Elimu Mkoa
wa Rukwa Samson Hango kuhakikisha timu anayoingoza inajipanga kuchukua hatua
kali za kinidhamu na kisheria kwa walimu wote wanaoshabikia mimba za utotoni
kwenye maeneo yao.
Katika
hatua nyingine Mkirikiti ameagiza vijana wa skauti kote mkoani Rukwa kutumika
na halmashauri kubaini wazazi wanaotekelekeza watoto na kusababisha wahamie
mitaani na kuitwa ’watoto wa mtaani’ ambao wanazidi kuongezeka hususan Manispaa
ya Sumbawanga.
Kwa
upande wake Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Sebastian Waryuba alisema atahakikisha
anashirikiana na vijana hususan skauti kufundisha vijana umuhimu wa maadili
mema ili waweze kuwa raia wema na kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi.
Waryuba
aliongeza kusema jamii inatakiwa kuelimishwa juu ya umuhimu wa uzalendo hatua
itakayosaidia kuwa na jamii bora itakayochukia maovu ikiwemo rushwa.
Mwisho.
Comments
Post a Comment