Bodi Ya Bonde La Maji Ya Ziwa Tanganyika Kuweka Alama Kwenye Maeneo Ya Mwambao.

Bodi ya Bonde la maji ya ziwa Tanganyika imezuia kuendelezwa kwa ujenzi wa makazi ya wananchi kandokando ya ziwa Tanganyika na kupiga malufuku wakandarasi kuendesha shughuli za ujenzi wa miradi mikubwa ya serikali kwenye maeneo ya ziwa bila kuwa na vibali vya matumizi ya maji kutoka kwenye mamlaka husika.


Ziwa Tanganyika lina urefu wa km 673 na upana wa km72 huku eneo lote likiwa na km2 za eneo 32,900 na ujazo wa km3 18,800 huku urefu wa ufukwe ukiwa ni km 1,828.

Licha ya hilo ziwa Tanganyika limezungukwa na nchi ya Tanzania, kongo, Burundi na Zambia huku wananchi kutoka sehemu zote za nchi hizo wakilitegemea katika shughuli za uvuvi na usafiri.

Licha ya uwepo wa ziwa hilo lakini bado kumekuwa na changamoto ya mabadiliko ya tabia ya nchi, ambapo kwa mwaka 2020 /2021 kumekuwa na mabadiliko ya kupwa na kujaa kwa ziwa hilo na kusababisha madhara kwa wananchi pamoja na serikali kuingia hasara kubwa kutokana na miradi yake kuharibika.

 Hata hivyo kuongezeka kwa ziwa Tanganyika kumesababisha bodi ya maji ya ziwa Tanganyika kutembelea maeneo yote yalioathiriwa na maji ili kuona madhara kwa ujumla.

Akiongea wakati wa kutembelea bandari ya Kasanga pamoja na soko la samaki Kasanga, Mwenyekiti wa bodi ya maji ya ziwa Tanganyika Juliusi Shilungushela, alisema bodi hiyo ilitembelea maeneo yote ya mwambao wa Ziwa Tanganyika ili kuona madhara kisha kutoa ushauri wa kukabiliana na Ongezeko la maji hayo.

Kwa upande wake Ogamba Koneli kutoka ofisi za bonde la maji ya ziwa Tanganyika, alisema bodi imeazimia kuweka alama katika maeneo yote yanayozunguka ziwa hilo ili kusaidia wananchi kutofanya ujenzi pindi maji yanapo kuwa yakipungua.

Hata hivyo hivi karibuni Mkurugezni Mtendaji wa Halmashauri ya Kalambo Msongela Palela, alitembelea maeneo yote yaliotengwa na wananchi wa vijiji vya Kasanga na Kilewani kwa ajili ya ujenzi wa soko jipya la samaki baada ya soko la awali kuzingilwa na maji ya ziwa Tanganyika.

Hata hivyo Mkurugenzi huyo alibainisha kuwa serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi million 150 kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa soko hilo na kubainisha kuwa million 78 zimetengwa na wizara ili kusadia kazi hiyo.

 

Comments