KATIKA PICHA KATI KATI NI MKUU WA MKOA WA RUKWA JOACHIM WANGABO AKIZINDUA MKAKATI WA KUPAMBANA NA MIMBA ZA UTOTONI KWA WANAFUNZI.
Na Baraka Lusajo-Rukwa.
KATIKA kuhakikisha jamii inawalinda watoto dhidi ya vitendo
vya
ukatili vinavyopelekea mimba za utotoni,ulawiti,lishe duni na elimu bora,mkoa
wa Rukwa umejipanga kuwa ifikapo mwaka 2025 vitendo hivyo vinamalizika.
Mkakati mkuu uliopangwa na mkoa huo ni kutetea maslahi ya watoto
ili kuhakikisha wanapata elimu na kupatiwa mahitaji muhimu pasipo
kunyanyaswa,ambapo pia viongozi mbalimbali wa serikali na taasisi zote kuhakikisha
inalipa kipaumbele suala la maslahi ya watoto.
Mkuu wa mkoa wa Rukwa Joachim Wangabo katika kuhakikisha suala
hilo linafanikiwa amewaasa wananchi kuwachuja watu wanaogombea nafasi
mbalimbali za uongozi na wawachague wale wenye sera za kutetea maslahi ya
watoto pamoja na haki zao.
KATIKA PICHA NI BAADHI YA WANAFUNZI WAKIWA KWENYE MAADHIMISHO YA MKAKATI WA KUPINGA UKATILI . |
Wangabo alisema kuwa msingi bora wa makuzi ya mtoto ni elimu na
mkoa wa Rukwa wenye vijiji 339 na Kata 97, kuna vijiji 59 havina shule za
msingi na kata 25 hazina shule ya Sekondari hali inayowapelekea wananfunzi
kutembea umbali zaidi ya kilometa 5 kwenda shule hali inayosababisha kurubuniwa
kwa wepesi.
Alisema sababu kubwa ya watoto kutembea umbali mrefu
unasababisha kushawishiwa na hatimae kupata mimba za utotoni na kuongeza kuwa
pamoja na vijiji na kata hizo kukosa shule viongozi wa maeneo hayo wapo ikiwemo
maafisa watendaji wa vijiji na kata, madiwani na wabunge pamoja na viongozi wa
vyama vyote vya siasa.
“Mwaka jana tumefanya uchaguzi wa serikali za mitaa, sasa jukumu
lao la kwanza hawa viongozi na hao wengine ambao wanataka kuwa wabunge mwaka
huu, na madiwani wahakikishe kwamba hivi vijiji 59 vyote vinakuwa na shule ya
msingi, kampeni zenu kujipanga kwenu kote, piga ua jengeni shule za msingi
kwenye vijiji vyenu’’alisema Wangambo.
Aidha Wangabo aliwataka viongozi hao wa kuchaguliwa wahakikishe
kuna vyumba vya madarasa vya kutosha pamoja na madawati, hapo ili kuwatendea
haki wananchi,’’sio tunatafuta uongozi wakati huduma za jamii zimedumaa, hili
ni jukumu kubwa kwa yeyote yule anayetangaza nia au kwa anayetaka kubaki kwenye
nafasi yake ya ubunge na udiwani” alisisitiza.
“Watoto wanakaa kwenye nyumba ambazo sio rasmi kama mabweni au
hosteli wanapanga nyumba mitaan na wanajilea wenyewe hali ya kuwa ni watoto
wadogo ametoka darasa la saba ambaye miaka yote amekuwa akilelewa na wazazi
wake lakini ghafla anaanza kujilea mwenyewe, ajilishe ajipikie, aoge, ajilinde mwenyewe
tunawapeleka wapi hawa’’alihoji.
Aliongeza kuwa ili kudhibiti hali hiyo ni lazima tujenge
mabweni, tujenge shule za sekondari kwenye kata zote 25 hili ni jukumu jingine
la viongozi hawa wapya wa serikali za mitaa wakishirikiana na wakurugenzi,
madiwani na wabunge wanaotangaza nia ya kugombea.
Aidha,Wangabo amewaagiza wakuu wa wilaya kuhakikisha shule zote
zinatoa chakula shuleni bila ya kujali kama ni uji wa subuhi ama chakula cha
mchana na wafanye hivyo na kushirikiana na wakurugenzi, wazazi, kamati za shule
na kusisitiza kuwa viongozi hao watapimwa kila baada ya miezi mitatu na kila
mwaka ili watoto wapate chakula shuleni na kuzingatia elimu.
Wangabo aliyasema hayo katika sherehe za uzinduzi wa mkakati wa
miaka mitano (2020 - 2025) wa kukabiliana na mimba za utotoni katika mkoa wa
Rukwa jana tukio lililofanyika katika mji mdogo wa Namanyere, Halmashauri ya
Wilaya ya Nkasi na kuhudhuriwa na wabunge wa mkoa huo, Wakurugenzi, Wenyeviti
wa halmashauri pamoja na wadau wa maendeleo kwa mtoto ikiwemo Plan
International.
Wakati akisoma risala mbele ya mgeni rasmi kwa niaba ya watoto
wenzie mwanafunzi Alsiegarce Bernad alimuomba Mkuu wa Mkoa huyo kwa
kushirikiana na wadau mbalimbali kusimamia utekelezaji wa mkakati huo ili
watoto wa mkoa wa Rukwa waweze kupata haki zao stahiki na kuongeza kuwa kupitia
mwaka 2020 kuwa ni mwaka wa motto.
“Kuhakikisha mtoto anaweza kujifunza na kusaidia kazi za
nyumbani zisizo athiri elimu, afya na zinazoendana na uwezo wa mtoto, kuwalinda
watoto dhidi ya unyanyasaji, unyonywaji, kutelekezwa, kufanyiwa ukatili na
kuchukua hatua pale ambapo haki za mtoto zimevunjwa, kushirikiana na serikali
na wadau wengine katika kuhakikisha huduma zinapatikana kwa viwango stahiki
katika maeneo yao.” Alisema.
Halikadhalika katika uzinduzi huo ulitoka ushuhuda wa aliyekuwa
mwanafunzi Shule ya Sekondari Mtenga, Wilayani Nkasi ambaye alipata ujauzito
akiwa kidato cha nne na kukimbiwa na aliyempa ujauzito bila ya mafanikio ya
kumpata na hatimae alijifungua na hivi sasa anaendelea na ulezi huku
akitegemewa na mdogo wake anaemsomesha.
“Baada ya hapo mradi wa Plan ulifika pale Kijiji cha mtenga,
nilijiunga na kuchagua fani ya ushonaji, nilijifunza ushojani na nikajua na
tuliwezeshwa vifaa vya ushonaji, hadi sasa najua kushona najipatia fedha
zinazokidhi mahitaji yangu, hata hivyo nina mdogo wangu anasoma, na sasa hivi
ananitegemea mimi kuniomba fedha za matumizi shuleni, Namshukuru Mkuu wa mkoa
kutoa elimu juu ya utokomezaji wa mimba za utotoni, asanteni,” Alisema.
Kwa upande wake mbunge wa viti maalum wa CHADEMA mkoani Rukwa
Mh. Aida Khenan aliwataka wanafunzi wanaopata ujauzito wakiwa shuleni kutokata
tamaa kwani hata yeye ni muhanga watukio hilo wakati alipokuwa kidato cha tatu
na leo hii ni mbunge na hivyo kuwataka wananchi wa mkoa wa Rukwa kuungana
pamoja kutokomoeza mimba za utotoni.
“Mkutano sio wangu, Wilaya ni ya kwetu, mabadiliko ni ya kwetu,
wito wangu kwa wazazi, malezi ya mtoto yanaanza kwetu sisi wazazi, yanafuata
kwa mwalimu na jamii inayotuzunguka, Wilaya ya Nkasi tumekuwa kinara sasa kwa
mimba za utotoni katika mkoa wa Rukwa, sio sifa nzuri sana na sisi wenyewe wana
Nkasi tuna uwezo wa kufanya mabadiliko tukiongozwa na mimi mwenyewe na
wanankasi wengine, Kwasababu Rukwa ni pamoja na Wilaya ya Nkasi,” Alisisitiza
Awali akielezea mikakati ya shirika la Plan International kaimu
meneja wa shirika hilo mkoa wa Rukwa Kisasu Sikalwanda amesema kuwa shirika
limejipanga kuboresha elimu kwa jamii kupitia mijadala mbalimbali
itakayofanyika katika ngazi za kata kwa viongozi wa dini, viongozi wa kata,
wazee mashuhuri pamoja na watu maarufu kwa lengo la kuzungumza habari ya unyayasaji
na ukatili wa kijinsia unaoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini na
hasa katika mkoa wa Rukwa
“Leo hii tunakubaliana na wewe pamoja na mkakati huu unaokwenda
kuuzindua kwa jitihada mabzo tunatarajia kuzifanya na hasa mwezi huu wa tatu, tunataraji
kutoa elimu kwa kamati zisizopungua 33 katika kata mbalimbali katika mkoa wa
Rukwa na hatimae malengo yetu ni kuja kuwafikia viongozi mbalimbali takriban
660 kutoka kata 33 katika mkoa wetu wa Rukwa, Pia kama Plan International mwezi
wa tatu tunataraji kupata mradi utakaolenga kupambana na mimba za utotoni na
uzazi wa mapema” Alisema.
Awali akitoa maelezo mafupi juu ya mkakati huo Mganga mkuu wa
mkoa wa Rukwa Dkt. Boniface Kasululu alisema kuwa mimba za utotoni na uzazi
katika umri mdogo ni miongoni mwa changamoto zinazoukabili Mkoa.
“Takwimu za utafiti wa kidemografia za mwaka 2015-2016
zinaonyesha kuwa asilimia 29 ya wanawake wenye umri wa kuanzia miaka 15 hadi19
katika Mkoa tayari ni wajawazito au wameshazaa. Kiwango hiki ni kikubwa
ikilinganishwa na kiwango cha kitaifa ambacho ni asilimia 27. Tafsiri ya hali
hii ni kuwa, katika Mkoa wa Rukwa, Wanawake 29 kati ya wanawake 100 wenye umri
wa miaka 15 hadi 19 ni wajawazito au tayari wamezaa,” Alisema.
Na kuongeza kuwa sababu zinazopelekea mimba za utotoni ni pamoja
na kutokuwajibika kwa wazazi na viongozi katika suala zima la ulinzi na usalama
wa mtoto hasa mtoto wa kike, uelewa mdogo wa jamii kuhusu sheria zinazosimamia
masuala ya mahusiano ya watoto na wanafunzi, ukatili wa kijinsia, shinikizo rika,
idadi ndogo ya shule za bweni na idadi ndogo ya shule zinazotoa huduma ya
chakula cha mchana kwa wanafunzi.
Takwimu za matukio ya mimba za utotoni katika Mkoa zinaonyesha
kuwa, kwa kipindi cha miaka mitatu (2017 hadi kufikia Agosti, 2019), jumla ya
matukio 722 ya wanafunzi kupata mimba yaliripotiwa ambapo kati ya hao, matukio
171(24%) yalitokea katika Shule za Msingi na matukio 551(76%) yalitokea katika
Shule za Sekondari huku kwa mwaka 2019 peke kukiwa na mashauri 692 ya ukatili
dhidi ya watoto. Mwaka huu wa Mtoto unaongozwa na Kauli mbiu isemayo “Ulinzi
na Usalama wa Mtoto ni Jukumu la Kila Mmoja Wetu.”
Comments
Post a Comment