Soko Kuu La Samaki Kasanga Kuanza Kutumika Rasmi.


Na. Faustine Pius Ng'habi
Kalambo.
Mlipuko wa furaha, vicheko na ndelemo umeliteka eneo la mwambao wa ziwa Tanganyika kwenye ukanda unaomilikiwa na Wilaya ya Kalambo. Hii ni kufuatia tukio la Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Kalambo Msongela Palela kufanya kikao  na wavuvi, wakiwemo  wafanyabiashara wa samaki na kuazimia kuanza kutumika kwa soko la samaki la Kasanga mara moja kuanzia sasa ili lilete tija kwa wananchi na Halmashauri kwa ujumla.

Soko la samaki la Kasanga ni moja kati ya masoko mawili likiwemo soko la kimataifa la mazao lililoko Matai, masoko yaliyojengwa kuanzia mwaka 2009 hadi 2011 kupitia MVIWATA [Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania], ujenzi wake ukifadhiliwa na jumuia ya Ulaya kwa asilimia 80  na asilimia 20 ya ujenzi huo ikitolewa na Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga kabla  Wilaya ya Kalambo haijamegwa na kuunda Halmashauri kamili ya Wilaya. Lengo kuu la mradi huu, ni kuwaunganisha Wakulima ili wawe na sauti moja katika kushawishi na kutetea maslahi yao kiuchumi, kijamii, kiutamaduni na kisiasa.

Soko hili liko umbali wa kilomita 73 kutoka Mji wa Matai ambao ndio makao makuu ya Wilaya ukilenga kuwanufaisha takribani watu 35,205 wa ukanda wa Ziwa Tanganyika na watu 238,000 kutoka maeneo mengine ya Wilaya ya Kalambo. ]o-Hali kadhalika, mikoa kama vile Mbeya,Iringa, Njombe na Ruvuma pamoja na nchi jirani za Zambia, Kongo D.R.C, Rwanda na Burundi ni fursa za Masoko ya samaki zinazo vuliwa kutoka Ziwa Tanganyika na kuuzwa kupitia soko la samaki la Kasanga.

Nikupitia ukweli huu kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo, inawatangazia wafanyabiashara wote wa samaki ndani na nnje ya mipaka ya Tanzania kufika kwa wingi soko la samaki la Kasanga ili wapate samaki wengi na wenye ubora wa kiwango cha kimataifa kwa ajili ya kukuza mitaji yao na maendeleo ya Kalambo na Taifa kwa ujumla. Samaki wanaopatikana kwenye eneo hili ni pamoja na Sangara, Kuhe, Mikebuka, Samaki wa mapambo, dagaa wakubwa na aina zingine nyingi za samaki

Comments