Mwalimu Wa Shule Ya Msingi Kisumba Kibindoni Kwa Tuhuma Za Kumpatia Ujauzito Mwanafunzi.''kalambo''


Na Mwandishi  wetu- Rukwa

Jeshi la  polisi wilayani Kalambo mkoani Rukwa inamshikilia mwalimu wa shule ya msingi Kisumba(jina limehifadhiwa) mwenye umri wa miaka 31 kwa tuhuma za kumpa mimba mwanafunzi wa shule ya sekondari Chisenga iliyopo wilayani humo.

Kwamujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Kamanda wa polisi mkoani humo Justine Masejo ilieleza kuwa mwanafunzi huyo mwenye umri wa miaka 18 alikuwa anasoma kidato cha kwanza katika shule hiyo.

Alisema kuwa mtuhumiwa huyo anadaiwa kuwa alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanafunzi huyo hadi kupelekea kumpa ujauzito.

Kamanda Masejo alisema kuwa mpaka sasa mkoani humo kuna jumla ya matukio 27 yaliyoripotiwa katika vituo mbalimbali vya polisi ambayo yanahusiana na wanafunzi kukatisha masomo baada ya kupewa ujauzito.

Alisema kuwa katika kesi hizo wanafunzi 20 ni wa shule za sekondari na saba ni shule za msingi na zipo katika hatua mbalimbali za upelelezi huku baadhi zimekwisha fikishwa mahakamani.

Kamanda huyo wa polisi alisema kuwa hivi sasa jeshi hilo la polisi lina endesha operesheni maalum ya kuwakamata watu wanaojihusisha na vitendo vya mapenzi na wanafunzi kwani wamekuwa ni kikwazo cha utekelezaji wa nia njema ya serikali ya kutoa elimu bila malipo ili wanafunzi wengi waweze kusoma mkoani Rukwa.

Alisema katika tukio hilo lililotokea hivi karibuni bado polisi wanaendelea na upelelezi na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani mara tu upelelezi utakapo kamilika.


Comments