Mama Mjamzito Na Mwanae Wafariki Dunia Baada Ya Kusombwa Na Maji Ya Mto Kalambo.

Mto Kalambo



Na  Baraka Lusajo.  Kalambo.

Kivuko  cha  mto Kalambo
MWANAMKE mjazito aliyefahamika kwa jina la  Maria Kalunde miaka(42) pamoja na mtoto wake Magreth Lui(9) wamekufa maji baada ya kutumbukia katika mto Kalambo kutokana na kuteleza katika kivuko cha miguu cha mto huo.

Tukio hilo limetokea juzi katika kijiji cha kasitu kata ya Sopa wilayani Kalambo  mkoani Rukwa wakati watu hao wakivuka katika mto huo

Akizungumzia tukio hilo mmoja wa wakazi wa kijiji hicho, Nobert Mwanawima alisema mwanamke huyo mjamzito pamoja na mtoto wake walikufa maji kutokana na eneo hilo kutokuwa na daraja la kuvukia kitendo kilichosababisha wananchi wa kijiji hicho kutengeneza kivuko cha miguu kinachokatisha mto kwa kutumia miti.

Alisema kuwa mwanamke huyo alipokuwa akipita katika kivuko hicho pamoja na mwanaye waliteleza na kuangukia mtoni, na kisha walianza kupiga  kelele za  kuomba msaada, lakini kwakuwa watu walikuwa mbali hawakufanikiwa kufika kwa wakati kuwasaidia.

''siku   moja baadaye walipata taarifa kuwa miili yao ilipatikana katika kijiji  jirani na wakazi wa kijiji hicho waliamua kufanya maziko, ndipo walipoamua kuchukua  msiba na kuusafirisha hadi kijiji cha Katete walipokuwa wakiishi mama huyo pamoja na mwanaye'' alisema.

Naye Jelemia  shigoma mkazi wa  kijiji cha  Kasitu , alisema kuwa kutokana na changamoto ya kutokuwa na daraja katika  eneo hilo watu  wamekuwa  wakifa maji kutokana na kusombwa na maji hali hiyo imekuwa ikijitokeza mara kwa mara katika nyakati za masika kwakuwa mto huo unakuwa umejaa maji.

Aliiomba serikali kuwajengea daraja katika eneo hilo ili kuepukana na vifo vinavyotokea mara kwa mara kwani wao wamekuwa hawajisikii vizuri kushuhudia watu wakipoteza maisha kila nyakati za masika.

Ofisa mtendaji wa kijiji hicho Gasper kateka ,amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuongeza kuwa hapo awali hali ilikuwa mbaya zaidi kwakua hakukua hata hicho kivuko lakini kilipatikana baada yawananchi  kujichangisha  fedha  kiasi  cha  shilingi 10,000 kila mmoja kwaajili ya kuwalipa mafundi waliokitengeneza.

Diwani wa kata hiyo Richad Kamagari ,alisema tatizo la vifo kutokana na kutumbukia watu mtoni limekuwa likijitokeza mara nyingi na yeye amekwisha toa taarifa katika baraza la madiwani la halmashauri ya wilaya ya Kalambo.

Kwaupande wake kaimu katibu tawala wa wilaya ya Klambo,Mahmood  Shauri amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa serikali itajitahidi kutatua changamoto hiyo inayowakumba wakazi wa kijiji hicho.

Comments