Halmashauri Ya Kalambo Ya Pitisha Bajeti Ya Bilion 36.4




 Na Baraka  Lusajo. Kalambo.

HALMASHAURI ya wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa imepitisha bajeti ya shilingi bilioni 36.4 katika mwaka wa bajeti 2020/2021.

Akisoma bajeti hiyo jana katika baraza la madiwani lililofanyika katika ukumbi wa mikutano wa chuo cha Makatekista uliopo mjini Matai, Afisa mipango wa halmashauri hiyo Eric Kayombo ,alisema kuwa katika bajeti hiyo halmashauri imepanga kukusanya mapato ya ndani shilingi bilioni 1.8.

Alisema kuwa fedha bilioni 27.0 zitatumika kwaajili ya mishahara, shilingi bilioni 5.6 zitakuwa kwaajili ya miradi ya maendeleo na shilingi bilioni 1.8 ni kwaajili ya matumizi mengineyo.

Katika kikao hicho mwenyekiti wa halmashauri hiyo,Daudi Sichone aliwaomba madiwani wa halmashauri hiyo kwa kushirikiana na wananchi wajitahidi kujenga vyumba vya madarasa pamoja na maboma kwaajili ya zahanati na vituo vya afya kwakuwa hivi sasa serikali inatoa hela kwaajili ya kumalizia.

Alisema kuwa vijiji ambavyo havijishughulishi wao watakosa maendeleo kwakua serikali inatoa fedha kukamilisha maboma ambayo bado, hivyo ni lazima wananchi waanze ndipo serikali imalizie.

Naye mkuu wa wilaya ya Kalambo Julieth Binyura aliwataka wananchi wanaoishi vijiji vilivyopo maeneo ya mpakani kuwa makini na wageni wanaoingia,wasiwapokee kiholela badala yake watoe taarifa kwa vyombo vya ulinzi.

Alisema kuwa katika kipindi hiki cha mwisho wa mwaka kuna sikuu hivyo watu wasio wema wanaweza kutumia fursa hiyo kuingia nchini na kufanya uhalifu.

Comments