Uchaguzi Wa Mitaa Uliosusiwa Na Wapinzani Wafanyika Huku Baadhi Ya Maeneo Wagombea Wa CCM Wakipita Bila kupingwa

KATIKA  PICHA  NI  MSIMAMIZI  WA  UCHAGUZI  WILAYANI  KALAMBO ERICK KAYOMBO

Wakazi wa wilaya ya Kalambo Mkoani Rukwa wamejitokeza kupiga kura, asubuhi ya siku ya Jumapili, huku ulinzi ukiwa umeimarishwa tangu kuanza kwa zoezi la kupiga kura.
Hata hivyo katika maeneo kadhaa zoezi likionekana kwenda vizuri , huku kwenye maeneo mengine zoezi halikufanyika kabisa kwa kile kilichoelezwa kuwa kulikuwa na mgombea mmoja tu ambaye amepita bila kupingwa.

Mfano katika wilaya ya Kalambo ambayo ilikuwa na vijiji  33 na vitongoji 78 vinayowaniwa,  katika  maeneo  mengi  wagombea wa chama cha CCM walipita bila kupingwa katika nafasi zote, isipokuwa katika  vitongoji vitano  pekee,kwa mujibu wa Msimamizi wa uchaguzi  wilayani Kalambo Elick Kayombo.


Katika  picha  ni Erck Kayombo , msimamizi  wa uchaguzi  Kalambo.

Hata hivyo pamoja na viongozi wakuu wa vyama vya upinzani kutangaza kususia uchaguzi huo, lakini wagombea wa baadhi ya vyama hivyo waliendelea kuwania nafasi mbalimbali katika baadhi ya maeneo wilayani  humo.

Uchaguzi huu hufanyika chini ya Ibara ya 8 (1) (a) ya Katiba ya Tanzania kuwa ni nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii na kuwa ndiyo msingi wa mamlaka yote iliyonayo serikali hupata kutoka kwa wananchi.
Vyama vilivyotangaza kujitoa kushiriki kinyang'nyiro cha uchaguzi huo ni Chadema, UMD, CCK, NCCR-Mageuzi, NLD, ACT-Wazalendo, CUF na Chauma.
Licha ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Seleman Jaffo, mwenye dhamana ya uchaguzi huo kutoa matamko mawili yenye nia ya kuviomba vyama vya upinzani kulegeza misimamo yao na kuwataka wagombea walioteuliwa kuendelea na uchaguzi huo, lakini hapakuwa na mafanikio yoyote.
Katika taarifa yake iliyokaririwa na vyombo vya habari nchini,Waziri Jaffo alivikosoa pia vyama vya siasa kwa kile alichokiita kushindwa kuwaelekeza wagombea wao namna nzuri ya kujaza fomu za kuomba kuteuliwa katika nafasi wanazogombea kwenye mitaa, vitongoji na vijiji.
"Inaonesha vyama vya siasa vilishindwa kuwasimamia wagombea wao wakati wa kujaza fomu hizo, kwa maana makosa mengine yalionekana ni kama ya mtu alijaza ili kushindwa mapema." Hilo alilitoa wakati anazungumzia suala la vyama vya siasa kujitoa kwenye uchaguzi huo, lakini vyama vilivyojitoa vilisimama kidete na kupinga mchakato mzima wa uchaguzi.

Comments