Serikali Wilayani Kalambo Yaanzisha Utaratibu Wa kuwatambua Wastaafu.


Na Baraka  Lusajo.Kalambo
Katika  picha  ni Katibu  Tawala wilayani  KalamboFrank Sichalwe.

Uongozi wa serikali wilayani Kalambo mkoa wa Rukwa umeanzisha utaratibu wa kuwatambua wastaafu wa utumishi wa umma ili kuwasaidia kupata haki zao na kujua taarifa za utumishi wao kwa ajili ya mahitaji ya lazima yanayojitokeza kwenye ofisi za umma wilayani hapa siku hadi siku.

Katibu tawala wa wilaya ya Kalambo, Frank Sichalwe, amesema kikao cha kwanza cha kuchagua viongozi wa umoja wa wastaafu wa utumishi wa umma wilayani humo kimebaini dosari za kiutendaji zinazokwamisha upatikanaji wa haki na stahiki zao kwa wakati.

Aidha ameelezea umuhimu wa kuunda umoja wa wastaafu wa utumishi wa umma kwa ajili ya kutatua changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika maisha yao mara baada ya kukoma muda wa utumishi wa umma.

Wakitoa hisia zao kupitia kikao kilicho jumuisha watumishi wastaafu wilayani Kalambo wameelezea jinsi wanavyokabiliwa na changamoto ya kupata haki na stahili zao ikiwa ni pamoja na kukabiliwa na vitendo vya kuombwa rushwa au kutapeliwa haki na stahili zao.

‘’tunaimani umoja huu utatusaidia kuondokana na vitendo vya utapeli kwani  baadhi yetu tumetapeliwa mara kadhaa na kuupongeza uongozi wa wilaya hiyo  kwa  kuunga mkono juhudi  zao’’.Walisema wastaafu hao.
Afisa utumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Kalambo Amandus Mtani amewataka wastaafu wote kufika kwenye ofisi yake pindi kunapotokea changamoto yoyote  kwa  lengo  la  kuitatua  kwa wakati.
‘’kimsingi wazee ni hazina ya jamii yoyote duniani na kwamba ni kundi muhimu linalo beba tunu na utamaduni uliotukuka kwa ajili ya maendeleo ya nchi hususani tanzania. hivyo Halmashauri itaendelea kutoa huduma kwa jamii na watumishi wote wakiwamo wasitaafu.’’alisema  Amandus Mtani.

Comments