WANANCHI WALIA KAMPUNI YA FABEC KUCHELEWESHA MRADI WA MAJI SONGWE




Na Ibrahim Yasini –Songwe.

WANANCHI wa vijiji vilivyopo kaya ya Mkwajuni makao makuu ya wilaya Songwe mkoani Songwe,wameiomba serikali kuharakisha ujenzi wa miradi ya maji kwenye kata na wilaya kwa ujumla inayosuasua kukamilika kwake licha ya serikali kutoa Bil.1.6.

Wilaya ya Songwe ni moja ya wilaya mpya mkoani Songwe iliyomegwa kutoka wilaya ya Chunya mkoani Mbeya miaka minne iliyopita,inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo ukosefu maji safi na salama inayosababisha watu kuugua homa ya kipindupindu kwa kunywa maji machafu ya mito na madimbwi.

Anna Kasole,mkazi wa Mkwajuni jana alisema serikali imepiga marufuku matumizi ya maji ya Madimbwi na ya mito ikiwemo mto Lulongo kutokana na madai kuwa maji hayo yanavimelea vya kipindupindu na kusema bado hawajawaonesha maji mbadala ya kutumia.

Getruda Pulumbu,mkazi wa mkajuni,alisema wamekuwa na kilio kikubwa juu ya ukosefu wa maji safi,lakini viongozi wa serikali na wa kisiasa wameuwa wakiwatoa hofu kuwa changamoto hiyo nitaondolewa lakini inaonekana kama ni ndoto kuondolewa.

Alisema mikutano mingi imefanyika ikitolewa pia ahadi nyingi za kuondoa tatizo hilo ambalo pia hata wakandarasi wa mradi waliletwa wakitangaziwa kuwa ndani ya miezi 6 watakamilisha ujenzi lakini hadi sasa bado ni kitendawili.

Juma Sambo,mkazi wa Mkwajuni,alisema siku za hivi karibuni katika mkutano wa hadhara ulioitishwa na mbunge wa jimbo hilo,walitangaziwa kuwa fedha zimetolewa tena za kimkakati zitakazoondoa tatizo la maji lakini hali ni tete.

Alisema kutokana na kunywa maji yasiyo salama,yamesababisha mamia ya watu kuugua kipindupindu kati ya hao 9 walifariki dunia,na sasa bado baadhi ya watu wanaendelea kutumia maji ya kwenyemito na madimbwi licha ya katazo kwa kuwa hawana sehemu mbadala ya kuchota.

Alfred Masuke,mganga mkuu wilayani humo,alisema kuwa watu 9 wamefariki dunia mwaka 2017-18 kwa kuugua homa ya kipindupindu na kuwa kwa sasa wamepiga marufuku matumizi ya maji ya mito lakini baadhi ya watu wanakaidi katazo hilo.

Kumekuwa na kawaida ya watu hasa kipindi ncha masika kufukua mchanga kwenye madimbwi na mito wakisaka maji na maji hayo yamepimwa na kubainika yanavimelea vya kipindupindu.

Abraham Sambila,mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo,licha ya kukiri kuwepo na changamoto hiyo,alisema walipokea fedha Bilioni 1.6 kwa ajili yamiradi ya maji lakini mkandarasi wa kampuni ya Fabec Investment aliyepewa tenda ya miradi hiyo anasuasua kukamilisha.

Alisema kutokana na hali hiyo,walimuandikia barua mbili za onyo na endapo hata kamilisha watamuandikia barua ya tatu ambayo ni ya kuvunja mkataba,hivyo aliwaomba wanannchi wawe watulivu kwani ifikapo Mwezi septemba mwaka huu miradi yote itakamilika.

Fillipo Mulugo,mbunge wa jimbo hilo,alisema ni kweli miradi hiyo imechelewa licha ya yeye kumuangukia katibu mkuu wizara ya maji kuomba fedha za kimkakati,lakini alisema walipomhoji mkandarasi alisema atakamilisha miradi hiyo ndani ya miezi 2 kuanzia sasa.

Kukamilika kwa mradi huo kutatatua kero ya maji ya muda mrefu,na wananchi pia wataondokana na hofu ya kuugua homa za magonjwa ya milipuko kikiwemo kipindupindu kilichoua watu 9 kufa na kadhaa kuugua.

Mwisho.



Comments