waziri wa kilimo na ushirika Japhet Hasunga akitembelea maghala ya mbolea . |
Waziri wa kilimo, Japhet Hasunga ameagiza
kukamatwa kwa kaimu mrajisi wa vyama vya ushirika mkoa wa Rukwa, Anyosisye
Mbetwa kwa tuhuma ya kushirikiana mmoja wa mawakala wa pembejeo za kilimo
kutapeli vyama vya ushirika zaidi ya Sh milioni 277.
Ametoa maagizo hayo hivi karibuni wakati akizungumza
na viongozi wa vyama vya ushirika (AMCOS) mkoa wa Rukwa kilichofanyika katika
ukumbi wa mikutano wa mkoa wa Rukwa mjini Sumbawanga.
Pamoja na mrajisi huyo, pia ameagiza kukamatwa
kwa wakala Elias Ndomba mkurugenzi wa kampuni ya Eli Agrovet Co ambao waliahidi
kufikishia mbolea kwa wakulima hao kupitia vyama vyao vya ushirika.
Waziri Hasunga alisema kuwa mrajisi huyo
ambaye ni afisa ushirika wa mkoa huo, kwa makusudi amekiuka sheria, kanuni na
taratibu za vyama vya ushirika hivyo amemshusha cheo hicho na sio afisa
ushirika tena.
Alisema afisa ushirika huyo amepoteza sifa ya
kuendelea kuwepo katika nafasi hiyo badala ya kuwasaidia wanaushirika yeye anashiriki
kuwahujumu.
"Naagiza hawa wote wakamatwe mara moja
kwa kuwa wamewatapeli sana ushirika kwa kuchukua fedha zao pasipo kuleta mbolea
labda wakileta mbolea hapa ndio waachiwe tofauti na hivyo wafunguliwe mashtaka
ya kuhujumu uchumi" alisema Waziri Hasunga.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa chama kikuu cha
ushirika cha Ufipa, Anastela Malaji alisema chama kwa niaba ya Amcos 49 kiliingia mkataba na
kampuni ya Eli Agrovet ya kusambaziwa mbolea kwa bei elekezi iliyotolewa na
serikali amedai kwamba mrajisi aliwataka watoe fedha asilimia 30 ya mbolea
waliokuwa wakihitaji.
Alisema makubaliano ilikuwa kampuni hiyo
iongeze fedha asilimia 70 kisha kununua mbolea na kuwafikishia wakulima lakini
baadae iligundulika haikuwa na mtaji huo, hivyo kuchukua fedha hizo hizo za
kwao kununua mbolea kiduchu aina ya Dap na kuwapelekea wakulima hao kinyume na
makubaliano yao.
Inasemekana viongozi wa Ufipa walihamisha
fedha kutoka katika akaunti yao iliyopo benki ya NMB kiasi cha sh milioni 277
na kupeleka katika akaunti ya Eli Agrovet iliyopo benki ya CRDB ili kusaidia
kampuni hiyo kupata mkopo na kuwasambazia wakulima mbolea kwa kadri ya mahitaji
yao.
Inaelezwa kuwa makubaliano baina ya chama
hicho na kampuni hiyo ilikuwa inunue mbolea ya Dap, Urea na Can na kusambaza
kwa wakulima ili waweze kuzalisha mazao yao kwa tija.
Aidha, Katibu wa Mpona Amcos kutoka wilayani
Nkasi mkoani Rukwa, Silvester Kapita alisema kuwa kutokana na kuwachangisha
wakulima fedha wanalazimika kuyakimbia makazi yao kwa kuwa wakulima wanahisi
viongozi hao ndio wamewatapeli fedha zao.
Alisema Desemba 11 mwaka huu, kampuni hiyo
iliwapatia mbolea aina ya Dap lakini kwa wilaya ya Nkasi hivi sasa hitaji lao
ni Urea kwa kuwa mahindi tayari yamekuwa marefu na yanaanza kuharibika.
Naye, Mwenyekiti wa Mtema Amcos,
Thiofili Kamili alisema wao mahitaji yao yalikuwa tani 555 za mbolea na
walichangishana Sh milioni 8 ambayo ni asilimia 30 lakini hawajapata kabisa
mbolea hiyo.
Alimuomba Waziri huyo kuona umuhimu wa
kuwasaidia kupata mbolea kwa kuwa fedha si hitaji lao kwa sasa.
Aidha, Ndomba alipopewa nafasi ya kuzungumza
katika kikao hicho alisema kuwa kuchelewa kwa wakulima kupata mbolea kwa wakati
ni kutokana na yeye kutopata fedha kwa wakati katika taasisi za kifedha.
Comments
Post a Comment