KATIKA PICHA NI MKUU WA MKOA WA RUKWA JOACHIM WANGABO |
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa
Mh. Joachim Wangabo ametoa siku sita kwa wakusanya mapato wa halmashauri nne za
mkoa huo ambao hawajawasilisha makunsanyo yao benki ili kuweza kusomeka katika
mfumo wa kukusanya mapato ngazi ya halmashauri(Local Government Revenue Collection
Information System – LGRCIS).
Amesema kuwa wadaiwa
hao wanatakiwa kurudisha shilingi 1,217,350,090.85 ya mapato ambapo hadi tarehe
23.9.2019 fedha hizo zinasomeka kwenye mfumo lakini bado hazijapelekwa benki na
hivyo kuhisiwa kuwa zimo kwenye mifuko ya wadaiwa hao huku halmashauri ya Wilaya
ya Sumbawanga ikiongoza kwa kuwa na deni kubwa la shilingi 695,288,837.45.
Ameyasema hayo katika
kikao maalum cha kuwasilishiwa taarifa ya hali ya mapato Mkoani humo
iliyofanywa na timu ya uhakiki na ufuatiliaji wa mapato ya ndani kwenye mfumo
iliyoongozwa na Katibu Tawala msaidizi seksheni ya serikali za Mitaa, kikao
ambacho kimehudhuriwa na wakurugenzi, wakaguzi wa ndani pamoja na maafisa
TEHAMA wa halmashauri.
“Hawa wadaiwa wote
hawa ambao majina yao ninayo hapa, wako wengi, wengi sana, ninawapa siku sita,
wadaiwa wote wawe wamerudisha fedha hizi, zote zirudi na siku kama hii wiki
ijayo jumanne wote waje hapa, ntakaa nao kikao, wawe wamemaliza madeni yao yote
na mifumo yenu yote muwe mmeikamilisha na katika kikao hicho kutakuwa na kamati
ya ulinzi na usalama wote tutakuwa hapa, sina mchezo na upande wa kukusanya
mapato, tusipokusanya vizuri inamaana hata ile 10% ya vijana, wanawake na watu
wenye ulemavu haitatolewa vizuri,” Alisisitiza.
Aidha, Alimuagiza
Katibu Tawala wa mkoa kuhakikisha anawalinda wakaguzi wa ndani ambao ndio jicho
la kwanza ndani ya halmashauri kabla ya kuingia kwa mkaguzi wa nje na kuwataka
wakaguzi hao kutokatishwa tamaa na mtu yeyote mwenye lengo la kujipatia
umaarufu wa kisiasa na kuongeza kuwa mapendekezo yanayotolewa na wakaguzi hao
ni wajibu kufanyiwa kazi kwa haraka ili kuepukana na hoja za ukaguzi kutoka kwa
wakaguzi wa nje.
Awali akitoa taarifa
ya uhakiki na ufuatiliaji wa mapato ya ndani kwenye mfumo wa kielektroniki,
Katibu Tawala msaidizi seksheni ya Serikali za Mitaa Albinus Mgonya alisema
kuwa miongoni mwa masuala yaliyobainika katika ukaguzi huo ilionekana kuwa kuna
tatizo kubwa la kuwepo kwa matumizi ya fedha kabla ya kupelekwa benki na mapato
mengine kuwepo kwenye mikono ya watu kwa muda mrefu hali ianyopelekea kujikopesha
na kushindwa kurudisha.
“Upo udanganyifu
kwenye baadhi ya vituo vya kukusanya mapato kama vile stendi za mabasi, Minada,
maegesho ya magari n.k ambapo watoa ushuru kwa maana ya wateja hawana uhitaji
wa risiti kulingana na uharaka wao kwenye kazi zao, pia kuna udhaifu kwenye
usajili wa POS (Point Of Sales Machine) ambapo baadhi ya halmashauri
zimebainika kusajili kwa jina la sehemu au cheo mfano VEO au WEO badala ya jina
la mhusika na kusababisha mdaiwa halisi kutojulikana na kuwajibishwa kisheria,”
Alisema.
Kwa upande wake
mkaguzi wa ndani wa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga Sigridi Mapunda
alioroddhesha changamoto kadhaa ikiwemo udhaifu wa utekelezwaji wa hoja
anazoziibua katika kazi yake ya ukaguzi, udhaifu katika ofisi ya mweka hazina
pamoja na afisa TEHAMA wa halmashauri kushindwa kushughulikia miamala
iliyolipwa ili kuweza kufutwa katika mfumo.
“Wale wakusanya
mapato, watendaji wa kata huwa hawawashi zile mashine na hivyo hufanya kazi
‘offline’ wanapokuja kuchukua bili huwa wanawasha muda mfupi mara ile miamala
inapofunguka wanapewa bili ambayo ni ndogo kwasababu miamala mingine inakuwa
bado haijafunguka lakini baadae katika mfumo madeni ya wale wakusanyaji
yanapanda kutokana na kufunguka kwa ile mialamala,” Alisema.
Hadi kufikia tarehe
23.9.2019 mapato ambayo hayajawasilishwa (defaulters) kwa Manispaa ya
Sumbawanga ni shilingi 45,454,992,68, Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ni
Shilingi 695,288,837.45, Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo ni Shilingi
255,883,853.32 na Halmashuri ya Wilaya ya Nkasi ni Shilingi 220,722,407.40.
Comments
Post a Comment